KATIBU Mkuu Wa Chama Mapinduzi (CCM) Daniel Chongolo amesema Chama hicho hakitawavumilia baadhi ya viongozi waliopewa dhamana ya kuwahudumia wananchi katika ngazi yeyote ile hapa nchini kuishia kulalamika badala ya kufanya kazi.
Chongolo ametoa kauli hiyo Januari 24, 2023 Jijini Dodoma wakati wa hafla ya mapokezi ya Sekretarieti Mpya ya Chama Cha Mapinduzi Taifa ambapo amasema kuwa kuna baadhi ya watendaji wameaminiwa na serikali ila badala ya kutimiza wajibu wao ya kuwatumikia wananchi wanaishia kulalamika tu.
"Vicheko vicheko bila utekelezaji havivumiliki na sasa tunaenda kuanza kazi kwa vitendo na kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM tukianza na Mkoa wa Morogoro tutakwenda mpaka ngazi ya shina na katika ziara zangu zote nataka niwaone wale viongozi wa Shina kwani wao ndio msingi wa Chama cha Mapinduzi," Chongolo.
Katibu huyo amesema kuwa Wananchi wanataka huduma sio maneno mfano afya,Maji,umeme,barabara, na elimu bora hivyo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo zote na zingine viongozi ni lazima watimize wajibu wao kwani Chama hicho hakipo tayari kumvumilia kiongozi ambaye hawezi kuchukua maamuzi binafsi kwa maslahi mapana ya watanzania.
"Hatutamfumbia macho kiongozi yeyote yule atakayeshindwa kuchukua maamuzi kwa wakati kwa ajili ya kutatua changamoto sisi tutamchukulia yeye kwanza maana hatuwezi kukaa kimya mpaka yeye atakapoamua maana 2025 tutakosa majibu ya kuwajibu watanzania hivyo nawaahidi kufanya kazi kweli kweli,".
Ameongeza kuwa "Mimi ni Chongolo ila Nikiwa hapa mimi ni Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi hivyo sitaki kuona viongozi watakaotusababishia maswali mengi kwa watanzania yasiyokuwa na majibu tunataka vitendo sio Maneno," Chongolo
Naye Katibu wa itikadi na uenezi Chama hicho ,Sophia Mjema amesema kuwa kwa nafasi aliyopewa anaenda kufanyakazi kwa mitazamo tofauti kwani kabla ya kwenda kwa wananchi lazima idara hiyo uelimishaji uwe sawa.
“Lazima mabalozi wetu wakajue wananchi wanataka nini lazima ndugu zetu tutakapokwenda kwa wananchi tutaenda mpaka ngazi za vitongoji tukajue wananchi wanataka nini,”amesema Mjema.

0 Comments