Zanzibar, Juni 2, 2026 – Kampuni ya mawasiliano ya Airtel Tanzania kupitia huduma yake ya Airtel Money imezindua ushirikiano wa kimkakati na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) unaolenga kuboresha huduma za malipo ya umeme wa mfumo wa TUKUZA kupitia njia za kidigitali.
Mpango huo unaojulikana kama “Airtel Money na ZECO – Tukuza Kidigitali” unawawezesha wateja kununua umeme kwa haraka, usalama na urahisi kupitia simu za mkononi bila kufika ofisini au vituoni.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar, Mhe. Seif Kombo Pandu, amepongeza hatua hiyo akisema ni muhimu katika kuimarisha uchumi wa kidigitali na kuboresha upatikanaji wa huduma za umma. Alisema umeme ni msingi wa maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo utalii, elimu, afya na biashara ndogondogo
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania, Bw. Andrew Rugamba, amesema huduma hiyo mpya itawezesha wateja wa TUKUZA kurejesha umeme ndani ya sekunde chache, hivyo kuongeza ufanisi na urahisi wa maisha ya wananchi.
Naye Meneja Mipango na Biashara wa ZECO, Bi. Aisha Omary, amesema ushirikiano huo ni sehemu ya mageuzi ya kidigitali yanayolenga kuondoa mifumo ya kizamani na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi wote.
Katika kuhakikisha mfumo huo unafanya kazi bila changamoto, Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), Bw. Arafat Ally Haji, ameahidi kuhakikisha mawakala wa Airtel Money wanakuwa na ukwasi wa kutosha ili kuimarisha mtiririko wa miamala bila kukwama.
Uzinduzi huu unatajwa kuwa ni hatua muhimu katika kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kupitia mifumo ya kifedha ya kidigitali Zanzibar.



0 Comments